OIE KUINUA SEKTA YA MIFUGO NCHINI
Kikao cha ana kwa ana kati ya Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Abdallah Hamis Ulega (wa pili kutoka kulia) na Uongozi wa Shirika la Afya ya Wanyama Duniani (OIE). Kutoka kushoto: Mwakilishi wa OIE Kanda ya Kusini mwa Afrika Samuel Wakusama, Rais wa OIE na Kamisheni ya Australia Mark Schipp na Mkurugenzi Mkuu wa OIE Monique Eloit na Mkurugezi wa Huduma za Mifugo wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi (wa kwanza kulia) Hezron Nonga.
NAIBU Waziri wa Mifugo na Uvuvi
Abdallah Ulega ameliomba Shirika la Afya ya Wanyama Duniani (OIE) kuisaidia Tanzania
kukabiliana na changamoto zinazoikabili katika sekta ya mifugo ambazo zinasababisha
nchi kushindwa kusafirisha mifugo na
mazao yatokanayo na mifugo kama vile nyama kwenda katika masoko ya nje ya nchi.
Maombi hayo yamewasilishwa leo
nchini Tunisia ambapo Naibu waziri Ulega amehudhuria Mkutano Mkuu wa 23 wa
Shirika la Afya ya Wanyama Duniani (OIE) Kamisheni ya Afrika, uliofanyika Mjini
Hammament nchini humo.
Mara baada ya mkutano huo, Ulega akiambatana
na Mkurugenzi wa Huduma za Mifugo wa wizara hiyo Hezron Nonga amepata fursa ya
kufanya kikao cha ana kwa ana na uongozi mkuu wa Shirika hilo la Afya ya
Wanyama Duniani (OIE) kwa kuzungumza na rais wa shirika hilo Mark Schipp,
Mkurugenzi Mkuu Monique Eloit na mwakilishi wa shirika hilo kwa Ukanda wa Nchi
za Kusini mwa Afrika Samuel Wakusama.
Ulega ameziainisha changamoto
hizo kuwa ni pamoja na magonjwa, kasi ndogo ya mifugo kuzaliana (Poor Breeding)
na uzalishaji duni (Low Productivity) ambapo kwa pamoja uongozi huo umeahidi
kuzifanyia kazi.
Mkutano huo uliojumuisha nchi
zaidi ya 25 za bara la Afrika zikiwemo Zambia, Zimbabwe, Misri, Kenya, Uganda,
Tunisia na Chad ulikuwa na malengo ya kuangalia afya ya wanyama, haki za
wanyama, uzalishaji wa mifugo na usalama wa chakula kitokanacho na mifugo na
kutoa mapendekezo kulingana na kanuni za shirika hilo duniani.
Katika mazungumzo hayo, Ulega
ameshukuru uongozi huo kwa ushirikiano wake na Tanzania kwa kuendelea kuisaidia
nchi katika miradi mbalimbali ya kulinda afya za wanyama hapa nchini.
Licha ya mazungumzo hayo, Ulega kupitia
kwa Mkurugenzi wa Huduma za Mifugo Hezron Nonga, amewakabidhi andiko
linalofafanua kwa kina sekta ya uvuvi nchini, changamoto zake na maeneo yenye
uhitaji ili kuuwezesha uongozi huo kuendelea katika hatua ya utekelezaji.
Pamoja na mambo mengine, Ulega
ameueleza uongozi wa OIE kuhusu nia ya Tanzania kuandaa mkutano ujao kwa kuwa
ni nchi yenye mifugo na wanyamapori wengi, mazingira mazuri ya uwezekaji na
taasisi maalum zinazoshughulikia masuala ya viwango, ubora wa bidhaa na usalama
wa chakula.
Katika kutathmini afya za
wanyama, wataalamu wamejadili magonjwa mbalimbali ya wanyama yaliyopo katika
bara la Afrika hususan kwa nchi wanachama, athari na namna yakuyakabili
yakiwemo magonjwa ya miguu na midomo (FMD), Kichaa cha mbwa na homa ya Bonde la
Ufa (RVF).
Aidha kikao kimetathmini kwa
pamoja miradi mbalimbali yenye lengo la kuimarisha afya za wanyama pamoja na
michango ya wahisani ikiwemo Benki ya Dunia, Mchango wa Wataalam wa Kati wa
Mifugo (Veterinary Paraprofessionals) na nafasi yao katika kuimarisha huduma za
afya ya wanyama katika Bara la Afrika.
No comments