JPM AISHUKURU CHINA KWA UHUSIANO NA USHIRIKIANO MZURI, NI KATIKA MAKABIDHIANO YA MAGARI 40 YA JWTZ.
Rais Dkt. John Magufuli
amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Watu wa China, Xi Jinping kwa kuuendeleza
ushirikiano na uhusiano mzuri wa Tanzania na China ikiwemo misaada na uwekezaji
ambao China inaufanya hapa nchini.
Rais Magufuli ametoa shukrani
hizo leo tarehe 12 Septemba, 2019 katika hafla ya makabidhiano ya magari 40
kutoka Jeshi la Ukombozi la Watu wa China (PLA) kwenda Jeshi la Ulinzi la
Wananchi wa Tanzania (JWTZ) iliyofanyika katika Makao Makuu ya JWTZ Upanga
Jijini Dar es Salaam.
Rais Magufuli amesema pamoja
kuisaidia Tanzania katika maeneo mbalimbali ya huduma za kijamii, ulinzi na
usalama na miundombinu, China ndio nchi inayoongoza kwa uwekezaji hapa Tanzania
ikiwa na miradi 723 yenye thamani ya takribani shilingi Trilioni 13.581 na
iliyozalisha ajira 87,126.
Ametaka uhusiano huo uimarishwe
zaidi kwa JWTZ na PLA kujenga kiwanda kikubwa chenye uwezo wa kubangua tani
laki 2 za korosho kwa mwaka, jambo ambalo litasaidia kuongeza thamani ya
korosho za wakulima wa Tanzania na kupelekwa China ambako kuna mahitaji makubwa
ya korosho.
Amemuomba Lut. Jen. Shao
Yuanming aliyeiwakilisha PLA katika makabidhiano ya magari hayo na Balozi wa
China hapa nchini Mhe. Wang Ke kufikisha shukrani zake kwa Rais Xi Jinping kwa
kuuendeleza na kuukuza zaidi uhusiano na ushirikiano mzuri wa Tanzania na China
na pia kufikisha ombi la kujengwa kwa kiwanda hicho.
Ameishukuru China kwa kutoa
msaada wa magari hayo 40 kwa JWTZ ambayo amesema yataimarisha utendaji kazi wa
jeshi hilo na pia ameomba PLA isaidie upatikanaji wa ndege kubwa za kubebea Askari
na vifaa kwa ajili ya jeshi hilo.
“Makabidhiano haya ya magari 40
ni kielelezo kingine tena cha uhusiano wa karibu, kidugu na kirafiki uliopo
kati ya Mataifa yetu mawili, tunaishukuru sana China kwa misaada mbalimbali
iliyoitoa kwa Tanzania.”
“China imekuwa mdau mkubwa wa
biashara kwa nchi yetu na pia inasaidia katika utalii, kwa mfano mwaka huu
tunatarajia kupata watalii 10,000 kutoka China” amesisitiza Rais Magufuli.
Kwa upande wake, Lut. Jen. Shao
Yuanming amemshukuru Rais Magufuli kwa kuhudhuria tukio hilo na kwa kuundeleza
na kuukuza uhusiano wa Tanzania na China ukiwemo uhusiano wa kijeshi na
ameahidi kuwa PLA itaendelea kushirikiana kwa ukaribu na JWTZ.
Nae Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi
Jen. Venance Salvatory Mabeyo ametaja baadhi ya maeneo ambayo JWTZ imenufaika
kutokana na ushirikiano wake mzuri na PLA kuwa ni pamoja na kujengwa kwa Kituo
cha Mafunzo ya Kijeshi huko Mapinga Wilayani Bagamoyo kilichogharimu shilingi
Bilioni 67, ukarabati na ujenzi wa uwanja wa ndege wa Ngerengere uliogharimu
shilingi Bilioni 137.63.
Ujenzi wa awamu ya 2 ya Chuo
cha Ulinzi wa Taifa Mkoani Dar es Salaam (NDC) utakaogharimu shilingi Bilioni
57 na kwamba kwa sasa PLA inakamilisha maandalizi ya kujenga Makao Makuu ya
JWTZ Mkoani Dodoma na kushirikiana na JWTZ katika zoezi kubwa la kijeshi
litakalofanyika hapa nchini kwa lengo la kubadilishana ujuzi katika ulinzi na
usalama.
Jen. Mabeyo amemuomba Lut. Jen.
Shao Yuanming kufikisha shukrani za JWTZ kwa uongozi wa juu wa PLA kwa msaada
wa magari hayo 40 na misaada mingine inayotokana na ushirikiano wa majeshi
hayo.
Pia, amemshukuru Rais
Magufuli kwa kuagiza JWTZ ipatiwe magari makubwa 12 yaliyokuwa yakitumiwa na
Bodi ya Dawa (MSD) ili yasaidie shughuli za jeshi.
No comments