WIZARA YA AFYA YAPATA BILIONI 26.6 KUTOKA SERIKALI YA UJERUMANI.
Katibu Mkuu Idara kuu Afya Dkt. Zainabu Chaula akisaini mkataba
huo wa shilingi bilioni 26.6 kutoka Serikali ya Ujerumani,halfa hiyo ilifanyika
kwenye ukumbi wa wizara uliopo mji wa serikali Mtumba.
Na. Catherine Sungura- Dodoma
SERIKALI kupitia Wizara ya Afya,
Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imesaini mkataba wa makubaliano wa
miaka mitatu na serikali ya Ujerumani kwa ajili ya kuimarisha afya ya msingi
nchini.
Akizungumza wakati wa kusaini
mkataba huo Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Dkt. Zainabu Chaula alisema kuwa wizara
yake imesaini mkataba huo na serikali ya Ujerumani katika kuboresha sekta ya
afya katika maeneo manne ambapo sekta hiyo itapata kiasi cha shilingi za
kitanzania Bilioni 26.6.
Dkt. Chaula amesema kwamba kwa
mwaka huu wameweka makubaliano ili fedha hizo zitolewe kwa wakati mmoja na
kuweza kutumia mfumo wa Force Akaunti kama walivyoweza kutumia kwenye ujenzi wa
Vituo vya afya na Hospitali za Wilaya na Mikoa katika kuboresha sekta ya afya
nchini.
“Tumeanza mahusiano tangu mwaka
1961, kuanzia mwaka 2003 huu ni mkataba wa tano na mkataba wao ni wa
miaka mitatu mitatu ambapo umejikita katika kuimarisha afya ya msingi katika
halmshauri zetu katika vituo vya afya pamoja na zahanati”.
Dkt. Chaula alitaja maeneo
yatakayonufaika na mkataba huo ni uhimarishaji wa taarifa, afya ya mama na
mtoto, uzazi wa mpango, bima ya afya kwa akina mama wajawazito pamoja na
utawala bora jinsi ya kutumia fedha hizi kulingana na kanuni na taratibu za nchi.
“Huu ni muendelezo wa mkataba wa
miradi mingi ambayo tumeifanya katika kuboresha sekta ya afya, kama
mnavyokumbuka hadi sasa hivi tumeshafanyia ukarabati wa vituo vingi vya afya
ambapo tuna vituo 470 ambavyo vimeshafanyiwa ukarabati tangu mwaka 2017
katika ngazi za zahanati, vituo vya afya na hospitali za wilaya.
Aidha, Dkt. Chaula alisema
Serikali iliwekeza shilingi bilioni mia moja na milioni mia tano katika
hospitali za halmashauri.
“Zamani hawa wenzetu walikua
wakitumia wakandarasi wao na pesa wanakaa nazo hivyo tumekaa nao na kukubaliana
kama fedha hizi watazitoa kwa wakati mmoja ili tuweze kuzisimamia kama
tulivyofanya kwenye vituo tulivyoanza ili kuweza kutekeleza kwa umakini na
kupata matokeo makubwa katika kipindi hiki” . Amesema Dkt. Chaula.
Kwa upande wa hali ya uzazi, mama
na mtoto Katibu Mkuu huyo alisema hivi sasa inakaribia asilimia 80 ya akina
mama wajawazito wanajifungulia kwenye vituo vya afya tofauti na zamani ambapo
kulikuwa na changamoto kubwa kwani wengi walikua wanajifungulia majumbani kwa
asilimia 39 na kufuatia na asilimia 59 hii ni kutokana na kuboreshwa kwa
vituo vya afya pamoja na mikakati mbali mbali ya kuhakikisha akina mama
wote wanajifungulia kwenye vituo vya afya.
No comments