Breaking News

WAZIRI BITEKO AKAGUA MIRADI YA MAENDELEO WILAYANI BUKOMBE

Waziri wa Madini Doto Biteko,

Tito Mselem Bukome,

Waziri wa Madini Doto Biteko, amekagua miradi ya maendeleo katika wilaya ya Bukombe mkoani Geita na kuwataka madiwani wilayai humo kutoa ushirikiano kwa watalamu ili kukamilisha miradi hiyo kwa wakati.

Waziri Biteko alitoa wito huo wakati alipotembelea miradi ya ujenzi wa madarasa katika shule ya sekondari Iguwa na shule ya msingi Mwalo zilizopo wilayani Bukombe.

Katika kutekeleza hayo Waziri Biteko alichangia vifaa vya ujenzi kwenye shule ya msingi Segwe, Mwalo pamoja na shule ya Sekondari ya Iguwa zilizopo wilayani humo ili kuharakisha ukamilishwaji wa shule hizo.

Waziri Biteko, alitoa mifuko 250 ya saruji katika shule ya msingi Segwe huku shule ya msingi Mwalo alitowa mifuko ya saruji 123 pamoja na kuchangia matofali zaidi ya 2500 katika shule ya sekondari Igewa ili kukamilisha ujenzi wa madarasa katika shule hizo.

Pamoja na mambo mengine, Waziri Biteko aliwataka Viongozi wa Kisiasa kusimamia miradi ya maendeleo kikamilifu na kuhakikisha wakati wa kampeni haukwamishi miradi kuendelea kujengwa, hayo aliyabainisha baada ya Diwani wa kata ya Igulwa Richadi Mabenga kudai kuwa wakati wa uchaguzi wa serikali za mitaa ujenzi ulisimama ili watu waingie kwenye michakato ya kisiasa.

Awali mkuu wa shule ya msingi Segwe Simon Sombi, alisema shule hiyo inawanafunzi 452 wasichana 227 wavulana 225 na kwamba wanafunzi wa darasa la pili walikuwa wanasomea chini ya miti kabla ya darasa la saba kuhitimu kutokana na upungufu wa madarasa.

Sombi alimushukuru Waziri Biteko kwa kuchangia hali ambayo itapunguza uhaba wa madarasa ingawa kunachangamoto zingine za upungufu wa nyumba za walimu.

Pia, Mkuu wa shule ya msingi Mwalo Makoye Ludubala, alishukuru mchango wa Waziri Biteko na kumhakikishia ufaulu mkubwa kwa wanafunzi katika shule hiyo.

“Shule ya Msingi Mwalo ina jumla ya wanafunzi 361 ikiwa wavulana 187 wasichana 174 na muhimu zaidi shule yetu imeshika nafasi ya kwanza kimkoa na ninakuahidi kuendelea kufanya vizuri katika mitihani ya kitaifa,” alisema Ludubala.

Kwa upande wake Muhandisi wa ujenzi wilaya ya Bukombe Dominico Shilingo aliunga mkono juhudi za Waziri Biteko na kuongeza kuwa hapa hakuna sababu ya kuchelewa kukamilika kwa mradi wa ujenzi wa vyumba nane vya madarasa katika shule ya sekondari ya Iguwa iwapo Diwani wa eneo hilo atatoa ushirikiano kwa watalamu na kuhamasisha wananchi kujitolea nguvu zao.

Muhandisi Shilingo alisema changamoto ya wataalamu kukosa ushirikiano kwa madiwani na wenyeviti wa mitaa ni kikwazo kikubwa kwenye maendeleo ya miradi hapa nchini.

Nae, Mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Bukombe Dioniz Myinga aliomba wananchi kuendelea kushiriki kwenye miradi ya maendeleo kwa kujitolea nguvu zao kwa kusomba kokoto, maji na mchanga ili kumuunga mkono Waziri wa Madini ambae ndiyo Mbunge wa Jimbo la Bukombe.

Mabenga alisema walifikia hatuwa ya kusimama kupisha uchaguzi wa serikali za mitaa na kwamba uchaguzi umeisha watahakikisha mradi unakamilika ifikapo Januari 2020 ili wanafunzi wa kidato cha kwanza waanze kutumia madarasa hayo.

No comments